• HABARI MPYA

    Wednesday, November 16, 2016

    SIMBA SC YAKUBALI KUTOA SH MILIONI 240 KUREJESHEWA OKWI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC imekubali kulipa dola za Kimarekani 120,000, zaidi ya Sh. Milioni 240 kwa klabu ya Sonderjiske ya Denmark ili kurejeshewa mshambuliaji wake, Mganda Emmanuel Okwi.
    Na baada ya Simba SC kulipa fedha hizo, Okwi atarejea kufanya kazi Msimbazi kwa mkataba wa mwaka mmoja kwa mujibu wa makubaliano hayo.
    Simba SC ilimuuza Okwi kwa dola 100,000 mwaka juzi Denmark, lakini kutokana na mchezaji huyo kutopata nafasi ya kucheza Ulaya, inaamua kumrejesha na makubaliano yamefikiwa.
    Emmanuel Okwi anatarajiwa kurejea Simba tena SC kwa dau la Sh. Milioni 240

    "Dola 120,000 tu wale jamaa wanataka watuachie Okwi. Na Okwi naye atasaini kwa mshahara tu mkataba wa mwaka huu, hatumpi dau la kusaini yeye,"kimesema chanzo kutoka Simba.  
    Okwi ni mchezaji aliyeipa faida kubwa Simba ndani na nje ya Uwanja enzi zake anacheza Msimbazi. Mbali na kuwasaidia Wekundu wa Msimbazi kushinda matajii mbalimbali tangu ajiunge nao kwa mara ya kwanza mwaka 2010, Okwi pia ameinufaisha kifedha Simba SC.
    Simba ilimuuza Okwi Etoile du Sahel ya Tunisia Januari mwaka 2013 kwa dau la rekodi kwa klabu za Tanzania, dola 300,000, ingawa baada ya muda akaingia kwenye mgogoro na klabu hiyo ya Tunisia.
    Mtafaruku ulianza baada ya Okwi kuchelewa kurejea mjini Sousse mkoani Sahel baada ya ruhusa ya kwenda kuichezea timu yake ya taifa, Uganda.
    Okwi naye akadai Etoile walikuwa hawamlipi mishahara na kufungua kesi FIFA (Shirikisho la Soka la Kimataifa), ambayo mwisho wa siku alishinda kwa kuruhusiwa kutafuta timu nyingine ya kuchezea kulinda kipaji chake, wakati wa mgogoro wake na klabu ya Tunisia.
    Okwi akajiunga na SC Villa ya kwao, Kampala katikati ya mwaka 2013 na Desemba mwaka huo, akahamia Yanga SC. 
    Hata hivyo, Okwi akavunja Mkataba na Yanga SC Agosti waka 2014, baada ya timu hiyo ya Jangwani kushindwa kumlipa dola za Kimarekani 60,000 kama ilivyokuwa katika Mkataba baina yao na kurejea klabu yake ya zamani, Simba.

    Na mapema Oktoba mwaka 2014, Simba SC nayo ilimuuza Okwi  SonderjyskE FC ya Ligi Kuu ya Denmark ambako alisaini Mkataba wa miaka mitano.
    Akiwa katika mwaka wa pili wa Mkataba wake wa miaka mitano, Okwi anatarajiwa kurejea Simba tena.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAKUBALI KUTOA SH MILIONI 240 KUREJESHEWA OKWI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top