• HABARI MPYA

    Thursday, November 17, 2016

    PLUIJM AKUBALI KUBAKI YANGA KAMA MKURUGENZI WA UFUNDI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    ALIYEKUWA kocha wa Yanga, Mholanzi Hans van der Pluijm amekubali kubaki klabuni kama Mkurugenzi wa Ufundi na ndiye atamshauri kocha mpya, George Lwandamina kuhusu muundo wa benchi la Ufundi.
    Habari za ndani kutoka Yanga zinasema kwamba Pluijm amekubali kubaki katika klabu kama Mkurugenzi wa Ufundi baada ya mazugumzo na uongozi wiki hii.
    Na kwa mujibu wa chanzi cha habari, Pluijm atakuwa na kikao na kocha mpya hivi karibuni, Mzambia Lwandamina kushauriana naye juu ya muundo wa benchi la Ufundi.
    Kuna uwezekano mkubwa waliokuwa Wasaidizi wa Pluijm ndiyo wakawa wasaidizi wa Lwandamina pia, kwa kuwa wote bado wana mikataba na hakuna shaka juu ya utendaji wao.
    Hans van der Pluijm (kushoto) amekubali kubaki Yanga kama Mkurugenzi wa Ufundi  

    “Mwambusi alidhihirisha uwezo wake mzuri tu baada ya kuiongoza vizuri timu kwa siku tatu ambazo Pluijm aligoma na akashinda mchezo dhidi ya JKT Ruvu 4-0,”kilisema chanzo.
    Lwandamina, beki wa zamani wa kimataifa wa Zambia aliyezaliwa Agosti 5, mwaka 1963 yuko Dar es Salaam tayari baada ya kusaini mkataba wa miaka miwili na anatarajiwa kuanza rasmi kazi mwishoni mwa mwezi huu.
    Wachezaji wa Yanga wamepewa likizo hadi Novemba 28 na kwa sasa Lwandamina anaandaa programu yake ya mazoezi.
    Kuhusu usajili wa dirisha dogo, ripoti ya kocha Pluijm ndiyo inasubiriwa ili kama imependekeza mchezaji wa kusajiliwa ifanyiwe kazi kwa kumshirikisha na kocha mpya.
    Pluijm mwenyewe hakuwa tayari kuzungumza chochote kuhusu mustakabali wake Yanga akisema; “Siko tayari kuzungumza chochote kuhusu mustakabali wangu kwa sasa na sitakuwa kuwa sehemu ya tetesi zinazoendelea,”.
    Hii ni awamu ya pili Pluijm kufundisha Yanga baada ya awali kufundisha kwa nusu msimu mwaka 2014, akimpokea Mholanzi mwenzake, Ernie Brandts kabla ya kwenda Uarabuni.
    Alikwenda Al Shoalah FC ya Saudi ya Arabia na nafasi yake ikachukuliwa na Mbrazil, Marcio Maximo ambaye naye alifanya kazi kwa nusu msimu kabla ya Pluijm kurejeshwa Januari mwaka jana. 
    Saudi Arabia ambako alikwenda na aliyekuwa Msaidizi wake, Yanga SC, Charles Boniface Mkwasa – Pluijm  aliondoka baada ya kutofautiana na uongozi wa timu uliotaka kumsajilia wachezaji asiowataka.
    Pluijm anaondoka Jangwani baada ya kuiongoza Yanga katika jumla ya mechi 128, akishinda 80, sare 25 na kufungwa 23.
    Katika mechi 19 za nusu msimu mwaka 2014, alishinda 11, sare sita na kufungwa mbili, wakati katika mechi 110 za tangu mwaka jana, alishinda 69, sare 19 na kufungwa 21.
    Msimu uliopita ulikuwa mzuri zaidi kwake, akibeba mataji yote matatu, Ngao ya Jamii, Ligi Kuu na Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Kombe la Azam Sports Federation (ASFC).
    Pluijm pia aliiwezesha Yanga kufika hatua ya makundi ya michuano ya Afrika (Kombe la Shirikisho) kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1998 na mara ya pili kihistoria. Yanga ilifika hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho mwaka huu baada ya mwaka 1998 kufika hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa.
    Na kwa mafanikio hayo, haikuwa ajabu Pluijm akishinda tuzo ya kocha bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara mwishoni mwa msimu uliopita. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: PLUIJM AKUBALI KUBAKI YANGA KAMA MKURUGENZI WA UFUNDI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top