• HABARI MPYA

    Friday, November 18, 2016

    NYASI BANDIA ZA SIMBA ZAKWAMA BANDARINI DAR

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    NYASI bandia za klabu ya Simba SC zimekwama bandarini mjini Dr es Salaam kutokana na klabu hiyo kushindwa kuzilipia kodi sasa.
    Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Ujenzi wa Uwanja Bunju Complex wa klabu hiyo, Zacharia Hans Poppe amesema leo katika mahojiano na BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE kwamba kwa sasa wanatafuta fedha wakalipie kodi na kuzitoa bandarini nyasi hizo.
    “Nyasi zimefika muda tu sasa, lakini tumeshindwa kuzitoa kwa sababu ya gharama za kodi za TRA (Mamlaka ya Mapato Tanzania). Tulijaribu kuomba msamaha wa kodi serikalini kupitia Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo, lakini tukanyimwa,”amesema Poppe.
    Hans Poppe amesema nyasi bandia za Simba SC zimekwama bandarini mjini Dr es Salaam  

    Aidha, Kapteni huyo wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), amesema kwamba kwa sasa yeye na Wajumbe wenzake wa Kamati hiyo wamejikita katika kutafuta fedha kwa namna nyingine ili wakalipie nyasi hizo.
    Poppe amesema kwamba kutokana na ugumu wa kupata fedha mapema, anasikitika deni litaongezeka kutokana na utaratibu wa ongezeko la ghrama kila siku baada ya wiki moja tangu mzigo wowote kuwasili bandarini.
    “Hatuna ujanja, kuna gharama zitaongezeka tu. Ndiyo maana pamoja na majukumu mengine tuliyonayo, lakini tunatafuta fedha kwa bidii,”amesema.  
    Mbali na Hans Poppe, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Wajumbe wengine wa Kamati ya Bunju Complex ni Salim Muhene, ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji kuwa Makamu wa Mwenyekiti.
    Katibu ni Issa Batenga wakati Wajumbe wa Kamati hiyo ni Ally Suru, ambaye Mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Adam Mgoyi ambaye pia ni Mjumbe wa Baraza la Wadhamini, Crescentius Magori, Imani Kajula na Jerry Yambi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NYASI BANDIA ZA SIMBA ZAKWAMA BANDARINI DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top