• HABARI MPYA

    Monday, October 17, 2016

    SAMATTA: UTEUZI HUU NI HESHIMA KWA NCHI YANGU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MWANASOKA wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta amesema kwamba kuingizwa kwenye kinyang'aniyo cha tuzo ya Mwanasoka Bora Afrika ni heshima kwa nchi yake.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY SPORTS - ONLINE leo, Samatta amesema kwamba amefurahi juu ya uteuzi huo, kwani anajiona anaendelea kuiwakilisha vyema nchi yake katika soka. 
    "Ni jambo kubwa na la kuvutia, najisikia furaha kwa kiasi kikubwa kuiwakilisha nchi yangu katika mchezo wa mpira wa miguu katika tuzo izi kubwa Afrika,"amesema msham uliaji huyo wa KRC Genk ya Ubelgiji.
    Mbwana Samatta (kulia) amesema kuingizwa kwenye kinyang'aniyo cha tuzo ya Mwanasoka Bora Afrika ni heshima kwa nchi yake

    Nahodha huyo wa timu ya taifa ya Tanzania, Samatta ni kati ya wachezaji 30 walioingia kwenye orodha ya awali ya kuwania tuzo ya Mwanasoka Bora wa Afrika pamoja na kipa Mganda, Dennis Onyango anayechezea Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini na kiungo Mkenya, Victor Wanyama anayechezea Tottenham Hotspur ya England.
    Orodha hiyo inaongozwa na Waalgeria watatu; mshambuliaji wa mabingwa wa England, Riyad Mahrez, Islam Slimani wa Leicester City na El Arabi Hillel Soudani wa Dinamo Zagreb.
    Mkongwe Samuel Eto’o anayechezea Antalyaspor ya Uturuki naye yumo kwenye orodha, pamoja na Mcameroon mwenzake, Benjamin Mounkandjo wa Lorient.
    Wengine ni Serge Aurier (Ivory Coast na PSG), Eric Bailly (Ivory Coast na Manchester City), Yao Kouasi Gervais ‘Gervinho’ (Ivory Coast na Hebei Fortune), Mohamed Salah (Misri na Roma), Mohamed El Neny (Misri na Arsenal).
    Wamo pia Pierre-Emerick Aubameyang (Gabon na Dortmund), Andre Ayew (Ghana na West Ham), William Jebor (Liberia na Wydad Athletic Club), Mehdi Benatia (Morocco na Juventus), Hakim Ziyech (Morocco na Ajax), John Mikel Obi (Nigeria na Chelsea), Kelechi Iheanacho (Nigeria na Manchester City).
    Wengine ni Ahmed Musa (Nigeria na Leicester City), Cedric Bakambu (DR Congo na Villareal), Yannick Bolasie (DRC na Everton), Sadio Mane (Senegal na Liverpool), Kalidou Koulibaly (Senegal na Napoli), Keegan Dolly (Afrika Kusini na Mamelodi Sundowns), Itumeleng Khune (Afrika Kusini na Kaizer Chiefs, Aymen Abdennour wa Tunisia na Valencia, Wahbi Khazri (Tunisia na Sunderland)  na Khama Billiat (Zimbabwe na Mamelodi Sundowns).
    Ikumbukwe Samatta ndiye anashikilia tuzo ya Mwanasoka Bora Anayecheza Afrika aliyotwaa Januari mwaka huu kufuatia kushinda taji la Ligi ya Mabingwa Afrika na TP Mazembe ya DRC mwaka jana na kuwa mfungaji bora wa michuano hiyo.
    Ni mafanikio hayo yalimfanya anunuliwe na klabu ya Genk iliyoizidi kete Lyon ya Ufaransa na klabu nyingine ziliokuwa zinataka huduma ya mchezaji huyo wa zamani wa Simba SC.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA: UTEUZI HUU NI HESHIMA KWA NCHI YANGU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top