• HABARI MPYA

    Friday, October 14, 2016

    MRISHO NGASSA ATAJA SABABU ZA KUCHAGUA JEZI NAMBA 7 FANJA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KIUNGO wa kimataifa wa Tanzania, Mrisho Khalfan Ngassa amesema kwamba amechagua jezi namba saba (7) katika klabu yake mpya, Fanja ya Oman kwa sababu ndiyo jezi ya kwanza kabisa kuvaa wakati anaibuka kisoka mjini Mwanza.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY SPORTS – ONLINE leo kutoka Muscat, Oman anakocheza kwa sasa, Ngassa alisema kwamba amevaa jezi tofauti katika klabu mbalimbali, lakini 7 inabeba kumbukumbu nzuri katika maisha yake ya soka.
    Mrisho Ngassa kwa sasa anavaa jezi namba Fanja ya Oman
    Mrisho Ngassa akiwa na jezi ya kwanza kuvaa katika maisha yake ya soka mjini Mwanza
    Ngassa (katikati) akiwa na Mtanzania mwenzake wanayecheza naye Fanja, Dannya Lyanga (kulia)

    “Wakati naibuka kisoka, nakumbuka jezi ya kwanza kuvaa ilikuwa namba saba katika timu yangu mtaani, Kirumba (Mwanza). Sasa nilipofika huku (Oman) moja kati ya jezi zilizokuwapo ni namba 7, nikaamua kuchagua hiyo kwa sababu hiyo,”alisema Ngassa.
    Ngassa alijiunga na Fanja mwezi uliopita kwa mkataba wa miaka miwili akitokea ya Free State Stars ya Afrika Kusini.
    Mchezaji huyo wa zamani wa Toto Africans ya Mwanza, Kagera Sugar ya Bukoba, Yanga SC, Azam FC na Simba za Dar es Salaam alijiunga na wawakilishi hao wa Oman kwenye Ligi ya Mabingwa ya Asia, aliondoka Free State mwezi uliopita baada ya kuomba mwenyewe kuvunja Mkataba.
    Ngassa alijiunga na Free State Stars Mei mwaka jana akisajiliwa na kocha Mmalawi, Kinnah Phiri kwa mkataba wa miaka minne.
    Hata hivyo, kocha aliyemsajili baba huyo wa Farida (9) na Faria (7) alifukuzwa baada ya miezi miwili tu na sasa tayari yuko Mbeya City ya Tanzania.
    Katika kipindi cha mwaka mmoja wa kuwa Free State, Ngassa alifanya kazi na makocha wanne akiwemo huyu wa sasa, Mfaransa Denis Lavagne aliyeanza kazi Juni mwaka huu.
    Wengine ni Mjerumani Ernst Middendorp aliyefanya kazi kati ya Septemba na Desemba 2015, Mtaliano Giovanni Solinas aliyefanya kazi kati ya Desemba na Mei 2016.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MRISHO NGASSA ATAJA SABABU ZA KUCHAGUA JEZI NAMBA 7 FANJA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top