• HABARI MPYA

    Friday, October 07, 2016

    BMT YASEMA HAITAMBUI YANGA KUKODISHWA KWA MANJI

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    BARAZA la Michezo la Taifa (BMT) limesema kwamba halitambui klabu ya Yanga SC kukodishwa kwa kampuni ya Yanga Yetu, kwa kuwa taratibu haazikufuatwa na Baraza la Wadhamini la klabu hiyo halitambuliki.
    Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mjini Dar es Salaam, Katibu wa BMT, Mohammed Kiganja amesema kwamba wao wanaendelea kutambua kama Yanga SC ni mali ya klabu na haijakodishwa kwa kampuni ya Yanga Yetu.
    Kiganja amesema kwamba, taratibu hazikifuatwa katika mchakato mzima ulioifikisha Yanga SC kwenye kukodishwa, hivyo zoezi hilo ni batili.
    “Hatupingi klabu zetu kufanya mabadiliko isipokuwa tunajaribu kuwakumbusha kufuata utaratibu wa kisheria na katiba zao. Kwa sababu unapobadilisha jina au kufanya marekebisho yoyote, ni lazima vikasajiliwe na kutambulika,”amesema.
    Aidha, Kiganja amesema hata Baraza la Wadhamini wa Yanga lilipitisha uamuzi wa kuikodisha timu, haitambuliki kwa Msajili wa Vyama na Klabu na Michezo wa BMT, kwa Wajumbe wake wengi ni wa muda.
    Amesema kati ya Wajumbe wa Baraza la Wadhamini la Yanga lililoundwa Julai 5, mwaka 1973 ni wawili tu wanaotambulika na walio hai hadi sasa, ambao ni Dk. Jabir Idrisa Katundu na Juma Mwambelo, wakati wengine wamekwishafariki dunia. 
    “Mwembelo pamoja na kwamba bado yupo hai, lakini kwa muda sasa hahusishwi tena mambo yanayoendelea ya klabu hiyo,” amesema.
    Kiganja amewataja Wajumbe wengine wa Baraza hilo la Muda, ambalo halikuwahi kusajiliwa wala kupitishwa kwenye Mkutano Mkuu ni Kapteni Mstaafu, George Mkuchika, Mama Fatuma Karume, Francis Kifukwe, Amri Ramadhan, Juma Kambi na Abeid Mohammed.
    Na akasema ili Yanga ikodishwe, inazotakiwa kwanza kifanyike kikao cha Kamati ya Utendaji itakayochambua hoja na kukubaliana au kutokukubaliana kabla ya kwenda kwenye Mkutano Mkuu wa wanachama, uwe wa dharura au kawaida na maamuzi yatakayofikiwa katika Mkutano yatapelekwa Baraza la Wadhamini, ambalo ndilo litawasilisha suala hilo kwa Msajili.
    “Sheria ya BMT ya mwaka 1967 kifungu namba 11 (1) kinasema chama chochote kinachofanya mabadiliko ya jina, anuani, madhumuni au kifungu chochote cha katiba yake kitatakiwa idhini ya Msajili. Kifungu namba 11 (3) Msajili anaweza kuyakataa maombi ya kubadili kifungu chochote cha Katiba kama ataona kuwa mabadiliko yanaweza kuhatarisha usalama na kuvuruga amani, au kama kuna malengo ya kuwanufaisha wachache au kama hayazingatii sera za michezo na sheria za BMT,” amesema Kiganja.
    Katibu huyo wa BMT amesema kwamba mchakato huo wa Yanga kukodishwa ungekuwa halali tu kama taratibu hizo zingefuatwa na kupita kote.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BMT YASEMA HAITAMBUI YANGA KUKODISHWA KWA MANJI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top