• HABARI MPYA

    Sunday, October 16, 2016

    AZAM NA YANGA LEO KUNA SHUGHULI KWELI SHAMBA LA BIBI

    REKODI YA YANGA NA AZAM FC: 
                        P   W   D   L   GF   GA   GD Pts
    Yanga SC   19   7    5   7   24    23    1    26
    Azam FC    19   7    5   7    23   24   -1    26

    MECHI ZILIZOPITA ZA AZAM NA YANGA:
    Agosti 17, 2016
    Azam FC 2-2 Yanga SC (Ngao ya Jamii, Penalti 4-1 Taifa)
    Mei 25, 2016
    Yanga 3-1 Azam FC (Fainali Kombe la ASFC)
    Machi 5, 2016 
    Yanga 2-2 Azam FC (Ligi Kuu Taifa)
    Januari 5, 2016 
    Yanga SC 1-1 Azam (Kombe la Mapinduzi)
    Oktoba 17, 2015 
    Yanga SC 1-1 Azam (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Agosti 22, 2015
    Yanga 0-0 Azam FC (Yanga ilishinda kwa penalti 8-7 Ngao ya Jamii)
    Julai 29, 2015
    Azam 0-0 Yanga SC (Azam ilishinda kwa penalti 5-3 Robo Fainali Kombe la Kagame)
    Mei 6, 2015
    Azam 2-1 Yanga SC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Desemba 28, 2014
    Yanga SC 2-2 Azam (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Septemba 14, 2014
    Yanga SC 3-0 Azam FC (Ngao ya Jamii)
    Machi 19, 2014; 
    Yanga SC 1-1 Azam FC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Septemba 22, 2013; 
    Azam FC 3-2 Yanga SC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Februari 23, 2013;  
    Yanga SC 1-0 Azam FC (Ngao ya Jamii)
    Novemba 4, 2012;  
    Azam FC 0-2 Yanga SC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Machi 10, 2012; 
    Yanga SC 1-3 Azam FC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    January 07, 2012
    Azam FC 3-0 Yanga SC (Robo Fainali Kombe la Mapinduzi)
    Septemba 18, 2011;  
    Azam 1-0 Yanga SC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Machi 30, 2011;  
    Yanga SC 2-1 Azam FC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Oktoba 24, 2010; 
    Azam FC 0-0 Yanga SC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Machi 7, 2010;  
    Yanga SC 2-1 Azam FC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Oktoba 17, 2009; 
    Azam FC 1-1 Yanga SC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Aprili 8, 2009;  
    Yanga SC 2-3 Azam FC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    Oktoba 15, 2008;  
    Azam FC 1-3 Yanga SC (Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara)
    (Rekodi hii inahusisha mechi za mashindano tu, tangu Azam na Yanga wanaanza kukutana)
    Mshambuliaji wa Azam FC, John Bocco akienda chini mbele ya beki wa Yanga, Vincent Bossou katika mechi baina ya timu hizo Agosti 17, mwaka huu

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inatarajiwa kuendelea leo kwa washindani wakuu wa taji hilo kwa misimu mitatu mfululizo iliyopita Azam na Yanga kumenyana.
    Timu hizo zinatarajiwa kumenyana leo katika mchezo namba 76 Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam, ambao utachezeshwa na refa mzoefu, Israel Nkongo wa Dar es Salaam pia. 
    Nkongo atasaidiwa na washika vibendera Soud Lila na Frank Komba, wakati refa wa akiba atakuwa Helen Mduma, wote wa Dar es Salaam pamoja na Kamishna Michael Wambura.
    Hiyo inakuwa mechi ya pili msimu huu baina ya timu hizo, baada ya Agosti 17, Azam kushinda kwa penalti 4-1 kufuatia sare ya 2-2 ndani ya dakika 90 kwenye mchezo wa Ngao ya Jamii. 
    Na kwa ujumla huo utakuwa mchezo wa tano kuzikutanisha timu hizo mwaka huu – kwani mbali na mechi hiyo ya Ngao ya Jamii, timu hizo pia zilikutana mara tatu katika mechi tatu za mashindano tofauti.
    Mei 25, Yanga iliichapa 3-1 Azam FC katika fainali ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Kombe la Azam Sports federation (ASFC), Machi 5, zilitoka sare ya 2-2 katika Ligi Kuu na Januari 5 zilitoka sare ya 1-1 katika Kombe la Mapinduzi.
    Kwa ujumla huo utakuwa mchezo wa 20 kuzikutanisha timu hizo katika mashindano yote tangu mwaka 2008 na katika mechi 19 za awali, kila timu imeshinda saba na kufungwa saba na kutoka sare tano.
    Yanga itaendelea kujivunia safu yake kali ya ushamuliaji inayoundwa na wapachika mabao kama Simon Msuva, Donald Ngoma na Amissi Tambwe, wakati Azam FC zaidi inajivunia uzoefu wa Nahodha wake, John Bocco ‘Adebayor’.
    Bocco ndiye kinara wa ufungaji mabao kwenye mechi dhidi ya Yanga, akiwa amefunga mabao 13 kwenye mechi zisizopungua 15.
    Lakini kikubwa zaidi ni kwamba timu hizo zinakutana zote zikiwa hazina mwenendo mzuri sana katika Ligi Kuu msimu huu hadi sasa, Azam ikiwa imekwishapoteza mechi tatu na Yanga imefungwa mechi moja.
    Makocha wapya wa Azam FC kutoka Hispania wanaoongozwa na Zeben Hernandez Rodriguez wanatakiwa kushinda leo ili kurejesha imani ya waajiri wao. 
    Bodi ya Wakurugenzi ya Azam kihistoria haijawahi kuwavumilia makocha kiasi cha hiki cha akina Hernandez – maana yake uvimilivu unaweza kuwashinda iwapo na leo timu itafungwa.
    Ikumbukwe Azam inayomilikiwa na Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa na familia yake inaingia kwenye mchezo wa leo ikitoka kufungwa 1-0 na Stand United.
    Na baada ya kufungwa na Stand United ambayo iliifunga na Yanga 1-0 Uwanja wa Kambarage, Azam FC iliamua kubaki Shinyanga kuweka kambi ya kujiandaa na mchezo wa leo.
    Kocha wa Yanga, Mholanzi Hans van der Pluijm nayeb anahitaji ushindi ili kujaribu kuzuia mpango wa mabadiliko ya benchi la ufundi la klabu hiyo. 
    Mechi nyingine za Ligi Kuu leo, Ruvu Shooting itaikaribisha Mbeya City Uwanja wa Mabatini mkoani Pwani. Mwamuzi wa mchezo huo atakuwa Rudovic Charles wa Tabora akisaidiwa na Samwel Mpenzu wa Arusha na Jeremina Simon wa Dar es Salaam. Kamisha wa mchezo huo atakuwa Idelfonce Magali wa Morogoro.
    Mtibwa Sugar ya Morogoro na Tanzania Prisons ya Mbeya nazo zitacheza Jumapili Oktoba 16 kwenye Uwanja wa Manungu mkoani Morogoro. Mchezo huo namba 78 utachezeshwa na Elly Sasii wa Dar es Salaam. Waamuzi wasaidizi ni Ferdinand Chacha wa Mwanza Lulu Mushi wa Dar s Salaam wakati mwamuzi wa akiba Nicolaus Makalanga wa Morogoro. Kamishna ni George Komba wa Dodoma.
    Mchezo mwingine wa Jumapili utakuwa kati ya Toto African ya Majimaji ya Songea kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza. Mchezo huo Na. 79 utachezeshwa na mwamuzi Shomary Lawi wa Kagera akisaidiwa na Abdallah Uhako wa Arusha na Julius Kasitu wa Shinyanga huku mwamuzi wa akiba akiwa Mathew Akrama wa Mwanza. Kamishna atakuwa Michael Bundala wa Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM NA YANGA LEO KUNA SHUGHULI KWELI SHAMBA LA BIBI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top