• HABARI MPYA

    Sunday, September 18, 2016

    SERENGETI BOYS YAILAZA 3-2 KONGO, NKOMOLA AFUNGA MAWILI PEKE YAKE

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    TIMU ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys imeshinda mabao 3-2 dhidi ya Kongo – Brazaville katika mchezo wa kwanza hatua ya mwisho ya mchujo wa kuwania tiketi ya fainali za U17 Afrika mwakani nchini Madagascar.
    Matokeo hayo yanaiweka njia panda kidogo Serengeti katika kuwania tiketi ya Madagascar, kwani wanatakiwa kwenda kuulinda ushindi huo mwembamba katika mchezo wa marudiano Oktoba 2.
    Mshambuliaji Yohana Oscar Nkomola aliifungia Serengeti Boys mabao mawili kipindi cha kwanza dakika ya 43 pasi ya na 45, yote kwa jitihada binafasi akifumua mashuti mazuri baada ya kuwatoka mabeki wa Kongo. 
    Kiungo wa Serengeti Boys, Mohammed Rashid Abdallah akimuacha chini beki wa Kongo
    Yohana Nkomola akimtoka beki wa Kongo, Ngaloukossy Jessy kabla ya kufunga bao la kwanza 
    Nkomola akikimbia kushangilia baada ya kufunga bao la pili la Serengeti Boys

    Kipindi cha pili, Kongo walibadilika kimchezo na kuongeza kasi ya mashambulizi langoni hadi kufanikiwa kupata bao.
    Walipata bao hilo dakika ya 71 kwa mkwaju wa penalty wa Langa-Lesse Percy uliotolewa na refa Nelson Emile Fred baada ya Mboungou Prestige kuchezewa rafu na Israel Patrick.
    Na ni wakati huo huo kipa Wa Serengeti Boys, Ramadhan Kambwili alipoumia nyama na kulazimika kutoka nafasi yake ikichukuliwa na Kevin Kayego.
    Issa Abdi Makamba aliyetokea benchi kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Nkomola, aliifungia Serengeti Boys bao la tatu dakika ya 83 kwa jitihada binafasi pia akimtoka beki wa pembeni wa Kongo kushoto kabla ya kufumua shuti la kitaalamu lililotinga nyavuni. 
    Bopoumela Chardon akaifungia Kongo bao la pili dakika ya 88 akimalizia krosi ya Ntota Gedeon kutoka kushoto.
    Kikosi cha Tanzania kilikuwa; Ally Msengi/Kevin Kayego dk73, Ramadhan Kambwili, Nickson Kibabage, Enrick Nkosi, Israel Mwenda, Shaaban Zubeiry, Asad Ali, Kevin Naftali, Ibrahim Ali/Muhsin Makame dk48, Yohana Nkomola/Issa Makamba dk65 na Mohamed Rashid Abdallah.
    Kongo – Brazaville; ObouuaExamish Yawn, Mebeza Craiche, Ntota Gedeon, Moundza Prince, Ngumbi Exau, Ngaloukossi Jessy, Kibakila Christ, Langa- Lesse Percy, Mboungou Prestige/Mountou Edoward dk89, Mantourari Aldo na Kiba Konde Rodrique/Bopoumela Chardon dk67. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERENGETI BOYS YAILAZA 3-2 KONGO, NKOMOLA AFUNGA MAWILI PEKE YAKE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top