• HABARI MPYA

    Thursday, July 14, 2016

    MTUPIE JICHO SAMATTA AKICHEZA EUROPA LEAGUE KWA MARA YA KWANZA LEO

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta leo anatarajiwa kuanza kucheza michuano ya Europa League, wakati timu yake, KRC Genk ya Ubelgiji itakapoikaribisha FK Buducnost Podgorica ya Montenegro katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Pili ya mchujo Uwanja wa Luminus Arena mjini Genk.
    Timu hizo zitarudiana wiki moja baadaye, yaani Julai 21, mwaka huu Uwanja wa Pod Goricom mjini Podgorica nchini Montenegro na mshindi wa jumla atasonga mbele.
    Samatta anatarajiwa kupangwa leo kwa sababu amefanya vizuri katika michezo ya kujipima nguvu kujiandaa na mashindano hayo ya pili kwa ukubwa kwa ngazi ya klabu Ulaya, akifunga mabao matatu katika mechi nne.
    Mbwana Ally Samatta (kulia) anaanza kazi Europa League leo

    Samatta alifunga bao moja katika ushindi wa 4-0 ugenini dhidi ya Lommel United Julai 2, akafunga pia bao moja katika ushindi wa 5-0 dhidi ya Bocholt Julai 1 na akafunga tena bao moja katika ushindi wa 3-0 Julai 2 dhidi ya ESK Leopoldsburg. 
    Kabla ya mechi ya hapo, Samatta aliichezea pia Genk katika mchezo wa kirafiki Juni 25, ikishinda 7-1 dhidi ya Unity Termien, lakini siku hiyo hakufunga.
    Ikumbukwe Samatta alijiunga na Genk kwa dau la Euro 800,000 akitoka kushinda taji la Ligi ya Mabingwa Afrika na Mazembe pamoja na kuwa mfungaji wa michuano hiyo na pia kushinda tuzo ya Mwanasoka Bora Anayecheza Afrika ya CAF.
    Na sasa anawania kuweka rekodi ya kuwa mchezaji wa kwanza wa Tanzania kucheza michuano ya Europa League, huku akiwa ana ndoto za kufanya makubwa zaidi Ulaya
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTUPIE JICHO SAMATTA AKICHEZA EUROPA LEAGUE KWA MARA YA KWANZA LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top