• HABARI MPYA

    Wednesday, February 03, 2016

    DRC YATINGA FAINALI, YAING’OA GUINEA KWA MATUTA

    JAMHURI ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) imetinga Fainali ya michuano ya Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN) baada ya kuifunga Guinea kwa penalti 5-4 kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 120 leo Uwanja wa Amahoro mjini Kigali, Rwanda.
    DRC iliyowatoa wenyeji, Rwanda katika Robo Fainali kwa kuwachapa mabao 2-1 baada ya dakika 120 pia, ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 103 kupitia kwa Jonathan Bolingi aliyemalizia pasi ya Guy Lusadisu.
    Hata hivyo, Guinea iliyowatoa Zambia kwa penalti 5-4 kufuatia sare ya 0-0 ndani ya dakika 120 pia, ilisawazisha bao hilo kupitia kwa Ibrahima Sory Sankhon dakika ya 120 akimalizia pasi ya Alseny Camara Agogo.
    DRC wamefanikiwa kwenda fainali ya CHAN baada ya kuitoa Guinea kwa penalti 5-4 leo Kigali

    Katika mikwaju ya penalti, Badou Bompunga, Mika Miche, Jonathan Bolingi, Doxa Gikanji na Elia Meschack wote walifunga upande wa DRC, wakati Ricky Tulengi na Jose Lomalisa Mutambala walikosa.
    Upande wa Guinea waliofunga penalti ni Ibrahima Sankhon, Aboubacar Leo Camara, Aboubacar Kile Bangoura na Daouda Camara, wakati Ibrahima Sory Bangoura, Mohamed Thiam na Mohamed Youla walikoa.
    DRC, mabingwa wa CHAN ya kwanza mwaka 2009 nchini Ivory Coast sasa watasubiri mshindi wa Nusu Fainali ya pili kesho kati ya Mali na Ivory Coast Uwanja wa Nyamirambo kuanzia Saa 10:00, ili wakutane naye katika fainali.
    Mali iliwastaajabisha wengi kwa kuwatoa mabingwa wa mwaka 2011, Tunisia kwa kuwachapa mabao 2-1, wakati Ivory Coast iliwatoa Cameroon kuwa kuwatandika mabao 3-0.
    Fainali na mechi ya kusaka mshindi wa tatu wa michuano hiyo ya nne, baada ya iIe ya 2009 Ivory Coast, 2011 Sudan na 2014 Afrika Kusini ambako Libya waliibuka mabingwa, zitafanyika Jumapili.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DRC YATINGA FAINALI, YAING’OA GUINEA KWA MATUTA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top