• HABARI MPYA

    Tuesday, January 05, 2016

    MTIBWA SUGAR YAPIGA HODI NUSU FAINALI, MAFUNZO YAPUNGA MKONO WA KWAHERI

    BAO pekee la mshambuliaji Said Rashid Bahanuzi, limetosha kuipa Mtibwa Sugar ushindi wa 1-0 dhidi ya Mafunzo katika mchezo wa Kundi B michuano ya Kombe la Mapinduzi, uliofanyika Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Bahanuzi ‘Spider Man’, mshambuliaji wa zamani wa Yanga SC, alifunga bao hilo dakika ya 12, akimalizia krosi ya kiungo hodari Ally Shomary. 
    Mtibwa Sugar imejiweka katika mazingira mazuri ya kwenda Nusu Fainali

    Katika mchezo huo uliokuwa mkali na wa kusisimua, Mafunzo ilipoteza nafasi ya kupata bao la kusawazisha baada ya kipa wa Mtibwa Sugar, Hussein Sharif 'Casillas' kudaka krosi iliyopigwa na Haji Abdi katika dakika ya 24.
    Mafunzo inapoteza mchezo wa pili sasa baada ya awali kufungwa 3-0 na Yanga SC na hivyo kupoteza matumaini ya kwenda Nusu Fainali, ikiziachia vita hiyo timu za Bara tupu, Azam, Mtibwa na Yanga SC.
    Kwa ushindi wa leo, Mtibwa Sugar ya kocha Mecky Mexime anayesaidiwa na mchezaji mwenzake wa zamani wa timu hiyo ya Manungu, Turiani, Morogoro inafikisha pointi nne kuelekea mchezo wa mwisho dhidi ya Yanga SC Alhamisi baada ya sare ya 1-1 na Azam FC katika mchezo wa kwanza.
    Mchezo wa pili wa kundi hilo leo, unafuatia sasa kati ya Yanga SC na Azam FC kuanzia Saa 2:15 usiku.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTIBWA SUGAR YAPIGA HODI NUSU FAINALI, MAFUNZO YAPUNGA MKONO WA KWAHERI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top